Jumatatu, 25 Agosti 2014

Rasimu ya Katiba inataja Tunu za Taifa: Ni nani kati yetu anayezijua!

Ndesyu Florian


KWA UFUPI

Ni dhahiri, ndiyo maana hata wakati wa kuandika au kutunga kanuni zinazosimamia Bunge hilo, wengi walipinga kwa mfano uamuzi wa mambo kufanyika kwa njia ya kura ya wazi,waking’ang’ania usiri, ambao hakuna shaka ndiyo unaozaa maovu ambayo baadhi ya wanaCCM wakiwamo viongozi wanatuhumiwa nao.
Nimeamua leo nianze kwa kueleza kitu kinachoitwa tunu. Tunaambiwa na wataalamu wa Kiswahili kuwa tunu ni kitu anachopewa mtu na mwingine kuwa niishara ya mapenzi, hidaya, zawadi, adia, hiba, azizi.
Tafsiri nyingine ya Kiswahili ya tunu inaeleza kuwa ni kitu ambacho ni adimu kupatikana na chenye kutumika kwa nadra.
Nimetumia maneno tunu baada ya kusoma rasimu ya pili ya Katiba na randama yake na kukutana na neno hili ‘Tunu za Taifa’.
Nimebaini kumbe kuwa Tunu za Taifa ni baadhi ya mambo ambayo yalijadiliwa siku nyingi, yalishapita baada ya kuwa yamejadiliwa na wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba kule Dodoma, lakini bila kufikia mwafaka.
Kumbe, nimebaini kuwa mgawanyiko ndani ya Bunge hili ambalo mara zote nimesema kuwa limegawanyika na kubakia vipande, mgawanyiko wake ulianzia hapo.
Hivyo, nimeamua nikumegee msomaji leo japo kidogo kile kilichoandikwa ndani ya rasimu, kuhusu tunu hizi za Taifa, kitu ambacho huenda wapo baadhi yenu ambao hamjawahi kukiona au hata kukisoma.
Kifungu hiki kinatoka Sura ya Kwanza ya Rasimu, Ibara ya 5: Tunu za Taifa. Sehemu A- inazungumzia Maudhui ya Ibara. Kifungu hiki kinasomeka:
Ibara hii ya Rasimu ya Katiba inapendekeza kuwa Utu, Uzalendo, Uadilifu, Umoja, Uwazi, Uwajibikaji na Lugha ya Kiswahili ambayo ni lugha rasmi ya Taifa, ziwekwe katika Katiba kuwa ndizo Tunu za Taifa.
Binafsi, sina ubishi wowote kuhusu azma nzuri ambayo Tume ya Mabadiliko ya Katiba, chini ya Jaji Joseph Warioba iliiona wakati ule wa kuandika mambo haya ambayo yameandikwa na kuitwa Tunu za Taifa kwamba yana manufaa.
Haya ndiyo yameandikwa kwenye rasimu ya pili na ambayo inajadiliwa kwa sasa ndani ya Bunge hili ambalo hakuna shaka limemeguka na kubakia vipande, halina tena mshikamano, sifa kuu ambayo imewatambulisha na kuwabeba kwa miaka mingi Watanzania.
Nimesikia kutoka kwa baadhi ya watu waliokuwamo ndani ya Bunge hilo kuwa wakati wa kujadili sura hii ya kwanza ya rasimu, ambako nimeambiwa kuwa wajumbe waligawanyika kwa kiasi kikubwa.
Kwa bahati nzuri, wakati ule, wajumbe wale wanaounda kundi la Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) walikuwa bado ndani ya kikao hiki, nimeambiwa kuwa suala la Tunu za Taifa liliwachanganya wengi, kisha likawagawa. Kwa ufupi, hawakukubaliana.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni