Jumatatu, 25 Agosti 2014

Arfi naye kwenda kortini kupinga Bunge la Katiba

Dodoma. Mjumbe wa Bunge Maalumu, Said Arfi amesema anakusudia kwenda mahakamani kupata ufafanuzi wa uhalali wa Bunge hilo kuachana na Rasimu ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba na badala yake kufanya kile alichokiita kuandika rasimu nyingine.
Katika taarifa yake jana, Arfi alisema hatua yake ya kwenda mahakamani inatokana na ukweli kwamba baada ya Bunge Maalumu kukataa muundo wa serikali tatu uliopendekezwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba, haiwezekani tena kujadili Rasimu ya Tume.
“Badala yake kinachofanyika kwa sasa ni kuandika rasimu nyingine ili iendane na muundo wa serikali mbili ambao ndiyo Chama cha Mapinduzi wanaoutaka,” alisema na kuongeza kuwa kinachofanyika sasa katika kamati ni mabadiliko makubwa ya Katiba ya sasa na siyo uandishi wa Katiba Mpya.
“Kimsingi, baada ya wabunge wanaotokana na vyama vinavyounda Ukawa kuondoka, ni kama sasa nyani amekabidhiwa shamba la mahindi lisilo na mlinzi. Kwa hali inavyokwenda kinachofanyika siyo kutengeneza Katiba Mpya, bali kufanya marekebisho makubwa katika katiba iliyopo,” alisema Arfi.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni